Watu wametumia mafundisho ya Yesu Kristo kubuni dini nyingi
zinazodai kuwa za Kikristo. Hata hivyo, Biblia inasema kwamba kuna dini moja tu
ya kweli ya Kikristo. Fikiria sababu tatu zinazotufanya tufikie mkataa huo.
Yesu alisema
kwamba anafundisha ile “kweli” na Wakristo wa mapema walisema dini yao ndiyo
ile “kweli.” (Yohana 8:32; 2 Petro 2:2; 2 Yohana 4; 3 Yohana 3) Hilo
linaonyesha kwamba wale wanaoendeleza mafundisho ambayo yanapingana na
mafundisho ya Yesu hawaendelezi Ukristo wa kweli.
Biblia inafundisha
kwamba Wakristo wote wanapaswa ‘kusema kwa upatano.’ (1 Wakorintho 1:10) Hata
hivyo, dini nyingi za Kikristo hutofautiana kuhusu mafundisho ya msingi kama
vile, maana ya kuwa Mkristo. Dini zote hizo haziwezi kuwa za kweli.—1 Petro
2:21.
Yesu alitabiri kwamba wengi wangedai kuwa
Wakristo lakini wakose kutii amri zake naye angewakataa watu hao. (Mathayo
7:21-23; Luka 6:46) Watu fulani wangeongozwa vibaya na viongozi wa kidini
ambao huchafua ibada ya kweli ili kuendeleza masilahi yao wenyewe. (Mathayo
7:15) Hata hivyo, watu wengine wangependelea Ukristo bandia kwa sababu
wangeambiwa mambo wanayotaka kusikia badala ya kweli ya Biblia.—2 Timotheo
4:3, 4.
Katika mfano wake kuhusu ngano na magugu, Yesu alitabiri
kwamba kutakuwa na uasi-imani mkubwa dhidi ya Ukristo wa kweli. (Mathayo
13:24-30, 36-43) Kwa muda mrefu, watu wangeshindwa kutofautisha kati ya
Wakristo wa kweli na Wakristo wa uwongo. Kama vile Yesu alivyotabiri,
uasi-imani ulisitawi baada ya mitume kufa. (Matendo 20:29, 30) Hata ingawa
huenda mafundisho ya waasi-imani yakatofautiana, aina zote za Ukristo bandia
‘zimegeuka kutoka kwenye kweli.’—2 Timotheo 2:18.
Pia Yesu alitabiri kwamba hatimaye tofauti kati ya Ukristo
wa kweli na wa uwongo ungeonekana waziwazi. Hilo limetukia katika siku zetu,
“umalizio wa mfumo wa mambo.”—Mathayo 13:30, 39.

No comments:
Post a Comment